Njia zitakazotumika Kilimanjaro Marathon 2015 zatajwa

Mbio za Kilimanjaro Marathon 2015 zitafanyika kwenye njia ile ile iliyotumika mwaka jana baada ya kupimwa na kuidhinishwa na shirikisho la riadha duniani. Njia hiyo ni mzunguko na imelenga kuwafanya wanariadha wakimie kwa raha na usalama zaidi bila tatizo la msongamano barabarani.

Akizungumzia njia hiyo Mkurugenzi wa Kilimanjaro Marathon, John Bayo amesema “Ni njia nzuri sana. Mbio za Full marathon zitaanzia uwanja wa Ushirika na kwenda kilomita kumi njia ya kuelekea Dar es salaam na kurudia njia hiyo kupitia geti la Chuo cha Ushirika. Wakati wanariadha wa kilomita 42 wanapita mbele ya geti, wale wa kilomita 21 (Tigo Kili Half Marathon) watakuwa mbele yao kwa takribani dakika 30 maana mbio yao inaanzia kwenye geti la Ushirika na kupandisha kuelekea Mweka kwa umbali wa kiomita 8”.

Baada ya kilomita 8, njia wataacha barabara ya lami kukimbia kwenye barabara ya vumbi kwa kilomita mbili kupitia mashamba ya kahawa ili kuipata Barabara ya Lema ambapo wataendelea kukimbia na kupita Shule ya Kimataifa ya Moshi na kutelemka kuelekea uwanjani. Bayo alisema kwamba njia nzima ina viburudisho vya kutosha pamoja na vituo vya maji na vile vile magari ya huduma ya kwanza.

Mbio za walemavu zitaanzia uwanja wa Ushirika na kuifata Barabara ya Kilimanjaro ambayo ni tambarare tupu na ina kivuli hadi Barabara ya Lema ambapo watageuza na kurudi Uwanjani wakiwa wamekamilisha kilomita 10.

John Addison, Mkurugenzi Mkuu wa Wild Frontiers, waandaaji wa mbio hizo alisema njia hiyo mpya itapendwa na wanariadha kwakuwa inapita maeneo yenye mandhari nzuri ya miti na mashamba na  njia hiyo haina msongamano na anaamini kwamba washiriki watakimbia kwa raha katika mbio hizo zitakazofanyika tarehe 1 Machi, 2015.

Aliongeza kuwa mbio ndefu la Kilimanjaro Premium Lager Marathon za kilomita 42 zitaanza saa 12.30 asubuhi kutokea uwanja wa Ushirika wakati mbio za Tigo Kili Half Marathon zitaanzia nje ya geti la Chuo cha Ushirika saa moja kamili asubuhi na kukimbia wakielekea Mweka na mbio yao itaishia hapo hapo uwanjani. Wakati huo huo mbio za walemavu za Gapco zitaanza saa 12.45 (saa moja kasorobo) kutokea uwanja wa Ushirika na huku mbio za kujifurahisha za 5 km Fun Run zikianza saa 1.45 asubuhi kwenye mzunguko wa YMCA na kumalizikia uwanjani.

Mbio za Kilimanjaro Marathon 2015 zinaratibiwa na Executive Solutions kwa kushirikiana na Riadha Tanzania, Riadha Kilimanjaro na Kilimanjaro Marathon Club huku zikidhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager, Tigo, GAPCO, Simba Cement, KK Security, Keys Hotel, TPC Sugar,  CMC Automobiles Ltd, RwandAir, FNB Tanzania, Kibo Palace Hotel, UNFPA na Kilimanjaro Water.

Leave a comment